Elimu kuhusu Afya ya Jamii

FAHAMU KUHUSU HOMA YA INI

UGONJWA WA HOMA YA INI NA MAMBO MUHIMU KUFAHAMU

 

 

Ini ni kiungo muhimu sana ndani ya miili yetu, hufanya kazi zaidi ya 500 ; moja ya kazi ni kuchuja na kuondoa sumu kutoka kwenye damu.

Kutokana na sababu mbalimbali kama pombe iliyopita kiasi, sumu kwenye damu au maambukizi; ini hupata shida na kuvimba na kushindwa kufanya kazi vizuri. Hii hali huitwa HOMA YA INI au HEPATITIS.

Katika maeneo yetu, bara la Afrika maambukizi ya virusi wa Homa ya ini ndio sababu kuu ya shida kwenye ini. Virusi vya Homa ya ini vipo vya aina 5 (A,B,C,D,E).

Aina mbili za virusi (B na C ) ndio sababu kuu za ugonjwa wa homa ya ini na husambaa kupitia damu na majimaji ya mwili.

Homa ya ini ni sawa janga linaloua kimya kimya kulingana na takwimu za vifo za dunia inakadiriwa Kirusi cha homa ya ini aina ya B pekee huua watu 600,000 hivi kila mwaka.

Kwa wastani zaidi ya watu bilioni mbili, yaani, asilimia 33 hivi ya watu wote ulimwenguni, wameambukizwa virusi vya HBV, na wengi wao hupona baada ya miezi michache. Watu milioni 350 hivi huendelea kuwa na virusi hivyo mwilini, wengi huishi bila dalili na kuendelea kuambukiza watu wengine

 

NAMNA GANI UNAWEZA KUAMBUKIZWA VIRUSI VYA HOMA YA INI (B NA C)…….?

Virusi vya homa ya ini B na C husambaa kupitia damu, shahawa au maji maji mengine ya mwili.

Virusi hivi vina uwezo wa kusambaa na kuambukiza mtu mara 100 zaidi ya virusi vya UKIMWI.

Njia hizi husambaza virusi hivi vya homa ya ini..:

Kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto
Mama aliye na maambukizi ya Hepatitis B kumuambukiza mtoto wakati wa kujifungua, iwapo hamna juhudi za kitiba za kuzuia maambukizi kuna uwezekano hadi asilimia 90 kwa mama kumuambukiza mtoto.

 

Kufanya mapenzi na mtu mwenye maambukizi ya virusi vya homa ya ini

Kuchangia vifaa vyenye ncha Kali kama sindano hasa kwa watumia madawa ya kulevya au wachora tattoo, miswaki

Kuongezewa damu ambayo ina maambukizi ya homa ya ini.


Virusi vya homa ya ini vinaweza ishi nje ya mwili kwa muda mrefu…

Tafiti zinaonyesha virusi vya homa ya ini vinaweza ishi nje ya mwili hadi kwa muda wa siku 7, bado vikiwa na uwezo wa kuambukiza mtu. Tafiti zimeonyesha hata iliyokauka huwa na uwezo wa kuambukiza virusi hivi.

 

 

 

 

NB : Iwapo kuna damu imemwagika inatakiwa isafishwe na chlorine au spirit ili kuua virusi 

NANI YUPO KATIKA HATARI ZAIDI YA KUPATA MAAMBUKIZI YA VIRUSI VYA HOMA YA INI?  

*  Watoto wachanga waliozaliwa na mama aliye na maambukizi ya virusi vya homa ya ini 

 *  Watu wanaofanya biashara ya ngono

*   Wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao

*   Watu wanaojidunga dawa za kulevya

*   Mtu mwenye mpenzi ambaye anaishi na maambukizi ya virusi vya homa ya ini

*   Wafanyakazi wa sekta ya Afya

*   Watu wa familia wenye ndugu anayeishi na maambukizi ya kudumu ya virusi vya homa ya ini

*    Wagonjwa wa figo wanaotumia huduma za kusafisha damu (dialysis)

  

UGONJWA WA VIRUSI VYA HOMA YA INI HUJA NA DALILI MBALIMBALI…..

   

Dalili za muda mfupi (acute hepatitis)

   

➡️ Dalili hizi za mwanzo hutokea ndani ya miezi 6 baada kuambukizwa virusi vya homa ya ini, hutokea kwa baadhi ya watu hazitokei kwa kila mtu.

Mgonjwa mwenye maambukizi ya virusi vya homa ya ini hujiskia kuumwa


* Hupoteza hamu ya kula

* Kichefuchefu na kutapika

* Mwili kuumaMkojo kuwa na rangi iliyokolea kama Coca-Cola

* Kupata manjano kwenye macho, vinganja vya mikono/kucha au mwili      mzima.


 

Kuna kundi dogo la wagonjwa wa homa ya ini hupata ugonjwa mkali wa ini na kusababisha ini kushindwa kabisa kufanya kazi pia huweza kusababisha kifo. Hii hatua huitwa “fulminant liver failure”.

 

Maambukizi ya kudumu ya virusi vya Homa ya ini (chronic hepatitis)

Watu wenye maambukizi ya kudumu ya virusi vya homa ya ini mara nyingi huwa hawana dalili, kadri muda unavyoenda virusi husababisha ini kusinyaa (cirrhosis) na kushindwa kufanya kazi vyema.

  

 

  


Pia Maambukizi ya virusi vya homa ya ini huchangia pia kupata Saratani ya ini.

 

 

Kwa nini ni muhimu kupima ili kujua kama una maambukizi ya virusi vya homa ya ini? ….

Watu wengi huishi na maambukizi ya virusi vya homa ya ini bila kufahamu. Kwa kawaida katika kipindi fulani cha maisha mtu 1 kati ya watu 3 huambukizwa virusi vya homa ya ini. Baada ya kuambukizwa, kuna kundi la watu hubaki na maambukizi ya kudumu ya virusi vya homa ya ini ambayo huwa hayana dalili yoyote na kuendelea kuua ini kimyakimya. Dalili huja kuonekana waziwazi miaka mingi baada ya mtu kuambukizwa. Huonekana wakati tayari ini limenyauka au lina kansa.

Hivyo Mtu aliye na maambukizi ya kudumu ya virusi vya homa ya ini aina B akianza matibabu mapema, anaweza kuzuia ini lake lisiharibike sana. Pia kwa wenye maambukizi ya virusi aina C matibabu ya dawa wiki 12 humaliza virusi vyote.

 

NANI ANAHITAJI KUPIMWA MAAMBUKIZI YA HOMA YA INI?  

 

 

Watu kutoka makundi yafuatayo ni sharti kupimwa kama wana maambukizi ya virusi wa homa ya ini……  

Watu wanaoishi kwenye maeneo yenye maambukizi ya virusi vya homa ya ini kwa zaidi ya asilimia 2. -Tanzania ni moja ya nchi zenye kiwango cha maambukizi ya virusi vya homa ya ini kwa wastani wa 5% hivyo watanzania wote ni muhimu kupima

* Watu wote wanaotumia dawa za kulevya na kujidunga

* Wafanyakazi katika sekta ya afya

* Watu wote wanaoishi na maambukizi ya virusi vya UKIMWI

* Watu wote ndani ya familia wanaoshi na ndugu aliyeambukizwa virusi vya homa ya ini

* Watu wote wanaotumia dawa za kufubaza kinga ya mwili (immunosuppressive therapy)

* Watu wote wenye ugonjwa wa figo wanahitaji kuanza dialysis

* Kina mama wajawazito wote

* Wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao.

 

UGONJWA WA HOMA YA INI HUWA NA MATOKEO MABAYA…..

Kwa wastani watu 25 kati ya 100 walioambukizwa virusi vya homa ya ini wakiwa watoto na 15 kati ya 100 waliopata maambukizi ya kudumu ya homa ya ini baada ya utoto hufariki wakiwa na umri mdogo kwa ugonjwa wa ini (ini kushindwa kufanya kazi) au saratani ya ini.


CHANJO YA DHIDI YA VIRUSI VYA HOMA YA INI

  

 

 

Chanjo dhidi ya homa ya ini hutolewa kwa watoto wote kama ilivyo kwenye mpango wa chanjo wa Taifa, pia hutolewa kwa watu wazima ambao hawajawahi kupata chanjo.

Chanjo hutolewa kwa njia ya sindano, ambapo huwa ni sindano 3; sindano ya kwanza hutolewa baada ya kupimwa kujua kama hauna maambukizi tayari, sindano ya pili hutolewa baada ya mwezi mmoja na sindano ya 3 baada ya miezi 6.

Makundi ambayo ni lazima kupatiwa chanjo ya homa ya ini

* Watoto wote

* Watu wote wanaotumia dawa za kulevya na kujifungua

* Watu wote wanaoishi na maambukizi ya virusi vya UKIMWI

* Watu wote ndani ya familia wanaoshi na ndugu aliyeambukizwa virusi vya homa ya ini

* Watu wote wanaotumia dawa za kufubaza kinga ya mwili (immunosuppressive therapy)

* Wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao

* Watu wote wanaoufanya biashara ya ngono

* Watu wote ambao wana mpenzi zaidi ya mmoja ndani ya miezi 6

* Watu wenye maradhi ya kudumu ya ini

* Watu wengine wote wanahitaji KUJIKINGA dhidi ya virusi vya homa ya ini  



read more
JUA UGONJWA WA KISUKARI,CHAZO CHAKE,DALILI NA TIBA YAKE

Magonjwa yasiyo ya kuambukiza ni magonjwa ambayo hayasambazwi kwa mtu mwingine kwa kuwa hakuna vimelea mwilini vinavyohusiana na magonjwa hayo. Magonjwa yasiyo ya kuambukiza ni kama ya moyo na mishipa ya damu, figo, saratani, kifua sugu, kisukari, magonjwa ya akili na mengine ya kurithi kama vile ugonjwa wa selimundu (Sickle Cell Disease).

Ripoti ya Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) ya 2013, inadai magonjwa yasiyo ya kuambukiza ndio chanzo kikubwa cha vifo ulimwenguni, yakifanya asilimia 63 ya vifo vyote kwa mwaka. Magonjwa yasiyo ya kuambukiza huua watu zaidi ya milioni 36 kila mwaka. Asilimia 80 ya vifo vinasababishwa na magonjwa hayo hutokea nchi zinazoendelea, Tanzania ikiwa miongoni mwa nchi hizo. Inakisiwa kuwa mwaka 2020 magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza yatasababisha asilimia 73 ya vifo vyote duniani na asilimia 60 ya ukubwa wa tatizo la magonjwa duniani.


Nchini Tanzania, katika mpango wa upimaji wa afya kwa magonjwa yasiyoambukiza jijini Dar es Salaam, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umebaini kuwa idadi kubwa ya wanaume wanapatwa na magonjwa hayo kuliko wanawake. Uchambuzi huo umeonyesha magonjwa yasiyoambukiza kama kisukari, shinikizo la damu na saratani zote ambazo zimekuwa chanzo cha vifo hivyo, huku serikali ikisema imeamua kuongeza juhudi za makusudi kupambana nayo.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mfuko wa Bima ya Afya, athari ya magonjwa yasiyoambukiza ni mara nne zaidi ya watu waliopo mijini kuliko vijijini, huku asilimia 12.8 ya wanaougua wakiwa wako mijini na asilimia 3.1 wako vijijini kutokana na mfumo wa maisha.

Uchunguzi mwingine uliofanywa na jopo la madaktari bingwa kuanzia mwaka 2011 hadi 2014 ulibaini asilimia 79 ya watanzania wazee waligundulika kuugua magonjwa ya kisukari, macho na shinikizo la damu. Pia walidai magonjwa hayo yamekuwa kikwazo cha maendeleo kutokana na kuwasumbua wazee na hata wenye umri wa kati ya miaka 40 na 50.

Kisukari ikiwa ni moja ya muuaji wa kimya kimya katika kundi hili la magonjwa yasiyo ya kuambukiza. Watu milioni 285 duniani kote wameathiriwa na kisukari ambayo ni sawa na asilimia 6.6 ya idadi ya watu wote ulimwenguni pia ikishika nafasi ya 5 kwa kusababisha vifo duniani.

Nchi zinazoongoza kwa idadi kubwa ya watu wenye kisukari ni China wagonjwa milioni 43.2, India wagonjwa milioni 40.9, Marekani wagonjwa milioni 25.8, Urusi wagonjwa milioni 9.6 na Brazil wagonjwa milioni 6. Nchi zenye idadi kubwa ya watu wazima wenye kisukari ni Nauru kwa asilimia 30, Bahrain kwa asilimia 25.5, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kwa asilimia 25, Saudi Arabia kwa asilimia 23.7 na Mauritius kwa asilimia 20.

KISUKARI NI NINI HASWA?

Sukari mwilini hutokana na vyakula pamoja na vinywaji tunavyotumia kila siku na hutumika kuupa mwili nguvu. Glukosi ni aina ya sukari ambayo huzipa chembe za mwili nishati. Hata hivyo ili glukosi iingie ndani ya chembe hizo inahitaji insulini. Insulini ni kemikali (Homoni) ambayo hutokezwa na kongosho (Pancrease).

Kisukari ni ugonjwa unaotokana na mtu kuwa na sukari nyingi kupita kiasi kwenye damu. Ugonjwa huo huvuruga utaratibu wa kuingiza sukari ndani ya chembe kutoka kwenye damu kwa kuwa chembe huhitaji sukari ili kupata nishati.

Ugonjwa wa Kisukari hutokea pale ambapo tezi ya kongosho inaposhindwa kutengeneza kichocheo (Homoni) aina ya insulin au pale mwili unaposhindwa kutumia vizuri kichocheo hicho na kusababisha kuongezeka kwa sukari (Hyperglycemia) au kushuka kwa kiwango cha sukari (Hypoglycemia). Ugonjwa wa kisukari unaweza kusababishwa na kuwa na kiwango kidogo cha insulin mwilini, mwili kutosikia kichocheo hicho au yote mawili.

TAKWIMU MBALIMBALI ZA UGONJWA WA KISUKARI


Kulingana na ripoti mbalimbali karibu watu milioni 316 ulimwenguni pote wana kiwango kikubwa cha sukari kwenye damu, ingawa wengi wao hawajui wana kiwango hicho. Kwa mfano, nchini Marekani pekee asilimia 90 ya watu wenye sukari nyingi kwenye damu hawatambui kama wana tatizo hilo. Ingawa asilimia 8.3 ya watu watu wa Marekani wana Kisukari ambayo ni sawa na watu milioni 25.8 na kufanya Kisukari cha 7 kusababisha vifo vya watu Marekani.

Mamilioni ya watu wana ugonjwa huo lakini hawana habari! Ni ngumu zaidi kutibu ugonjwa wa kisukari kwa kuwa mtu anaweza kuishi nao kwa muda mrefu kabla haujagunduliwa. Hiyo ndiyo sababu watu husema kwamba ugonjwa huo huua kimyakimya.

NINI CHANZO HASA CHA KISUKARI?


Ili kuelewa vyema ugonjwa wa kisukari ni muhimu kwanza kuelewa namna chakula kinavyovunjwa vunjwa na kutumiwa na mwili ili kuzalisha nguvu. Wakati chakula kinapoyeyushwa matukio kadhaa hutokea. Moja ni sukari inayoitwa glucosi ambayo ni chanzo cha nishati/nguvu mwilini huingia katika damu. Tukio la pili ni kiungo kinachoitwa kongosho (Pancrease) kutengeneza kichocheo cha insulini. Kazi ya insulini ni kuondoa glucosi katika damu na kuingiza katika misuli, seli za mafuta na ini, ambako hutumika kama nishati.

Watu wenye kisukari huwa na kiwango kikubwa cha sukari kwenye damu kuliko inavyotakiwa kwa sababu miili yao haiwezi kupeleka sukari kwenye seli za mafuta, ini na misuli ili ihifadhiwe kwa ajili ya kuzalisha nguvu. Hii ni kutokana na moja ya sababu zifuatazo, huenda kongosho zao haziwezi kutengeneza insulini ya kutosha au seli za mwili wao haziathiriwi na insini kama inavyotakiwa au sababu zote hizo mbili.

Main Symptoms of Diabetes FikraPevu.com
Kama wewe ni mnene kupita kiasi, hufanyi mazoezi kwa ukawaida au una watu wa ukoo walio na kisukari, huenda tayari una kiwango cha juu cha sukari kwenye damu. Ongezeko la sukari kwenye damu mbali na kuwa kisababishi cha kisukari, hali hiyo inahusianishwa na hatari ya kupatwa na ugonjwa wa akili uitwao 'DEMENTIA'.

Kula sukari nyingi sio sababu ya ugonjwa wa kisukari. Lakini lazima tuseme kwamba kula sukari nyingi si nzuri kwa afya yako kwani utaongeza uzito wa kuweza kuathiri uwezo wa mwili wako kujikinga na maradhi tofauti. Ugonjwa wa kisukari umeitwa kwa kufaa "ugonjwa unaoathiri kiini cha nishati ya mwili". Mwili unaposhindwa kutumia glukosi, mifumo mbalimbali ya mwili inaweza kuacha kufanya kazi au hata kusababisha kifo.

Ugonjwa wa Kisukari kitaalamu hujulikana kama 'DIABETES MELLITUS'. Jina 'Diabetes Mellitus' linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha 'kunyonya' na neno la Kilatini linalomaanisha 'tamu kama asali'. Maneno hayo yanafafanua vizuri sana ugonjwa huo, kwani maji hupita mwilini mwa mtu aliye na ugonjwa wa kisukari kana kwamba yananyonywa na mdomo na kupitia kwenye njia ya mkojo kisha kutoka nje ya mwili. Isitoshe mkojo huwa na ladha tamu kwa kuwa una sukari. Ndiyo sababu kabla ya kuvumbua njia bora za kupima ugonjwa huo, mbinu moja ya kutambua kama mtu ana ugonjwa wa kisukari ilikuwa kumwaga mkojo wa mgonjwa karibu na kichuguu cha sisimizi. Ikiwa sisimizi wangevutiwa na mkojo huo basi hilo lilimaanisha kwamba mkojo una sukari.

NI NANI ANAWEZA KUWA NA UGONJWA WA KISUKARI?

Watu walio katika makundi yafuatayo wana uwezekano mkubwa wa kupata ugonjwa wa kisukari:-

– Wenye uzito uliozidi,

– Wenye historia ya kuwa na wagonjwa wa kisukari katika familia zao,

– Wanawake waliozaa watoto wenye kilo 4 au zaidi,

– Watu wasiojishughirisha au wasiofanya mazoezi,

– Wenye shinikizo la damu,

– Wenye msongo wa mawazo na

– Wenye matumizi makubwa ya pombe na sigara.

Watu hawa wanashauriwa kupima sukari yao kila mwaka wakiwa na umri wa miaka 45 na kuendelea.

Kuna hatari kubwa ya kuugua ugonjwa huo ikiwa mtu ana mafuta mengi katika tumbo na kiuno chake kuliko katika mapaja yake. Mafuta katika kongosho na ini huvuruga uwezo wa mwili wa kudhibiti kiasi cha sukari kwenye damu.

Wavutaji wa sigara wanakabiliwa na hatari kubwa zaidi kwani zoea hilo hudhuru moyo na mfumo wa mzunguko wa damu na kubana mishipa ya damu. Kitabu kimoja kinasema kwamba asilimia 95 ya watu wanaougua kisukari ambao hulazimika kukatwa viungo ni wavutaji wa sigara.

DALILI ZA UGONJWA WA KISUKARI


~ Kunywa maji mengi kuliko kawaida na kusikia kiu kila wakati.
~ Kwenda haja ndogo mara kwa mara. Watoto kukojoa kitandani.
~ Kuwa dhaifu, kukosa nguvu na kujisikia mchovu kila wakati.
~ Kupungua uzito au kukonda licha ya kula vizuri.
~ Kusikia njaa kila wakati na kula sana.
~ Wanawake kuwashwa ukeni.
~ Kutoona vizuri.
~ Kupungua nguvu za kiume au hamu ya kujamiiana kwa wanawake.
~ Ganzi, kuchomwachomwa au kutohisi unapoguswa sehemu za miguu, viganja na vidole.
~ Miguu kuoza na hata kupata gangrini.
~ Kukaukwa na ngozi na pia kupata aina ya ngazi katika miguu.
~ Vidonda au majeraha sehemu yoyote ya mwili kutopona haraka.
~ Majipu mwilini.

Wenye dalili hizi wanashauriwa kupima sukari ili kubaini kama wana kisukari.

read more
Fahamu kuhusu virusi vya Corona na ugonjwa wa COVID-19

Fahamu kuhusu virusi vya Corona na ugonjwa wa COVID-19

Virusi vya Corona vimeingia Afrika Mashariki baada ya mgonjwa wa kwanza kuripotiwa nchini Kenya. Najua unaweza kuingiwa wasiwasi. Lakini usiogope.

 

Hiki ni kirusi cha aina gani?

 

Corona ni jamii kubwa ya virusi vinavyosababisha maradhi kwa wanyama na binadamu. Kwa binadamu, jamii kadhaa za virusi vya Corona vinafahamika kusababisha maambukizi kwenye njia ya hewa na mfumo wa upumuaji. Maradhi yaliyowahi kusababisha madhara makubwa kutokana na virusi vya Corona ni pamoja na MERS na SARS yaliyozuka mwanzoni mwa miaka ya 2000. Kirusi cha Corona kilichogundulika hivi karibuni kinasababisha ugonjwa unaofahamika kama COVID-19.

 

COVID-19 ni nini?

 

COVID-19 ni ugonjwa wa kuambukiza unaosababishwa na virusi vya Corona. Virusi hivyo vipya havikuwa vikifahamika hapo kabla na sayansi ya tiba. Na vilianzia nchini China mwezi Disemba mwaka 2019.

 

Dalili za Corona ni zipi?

 

Dalili kuu za Corona ni pamoja na Homa kali, Uchovu na Kikohozi kikavu na zinatokea taratibu. Dalili kubwa na inayoweza kutia hofu, ni mtu kukosa pumzi. Lakini isikutishe, ni mtu 1 pekee kati ya watu 6 walioambukizwa virusi vya Corona hufikia dalili hiyo ya hatari. Na asilimia 80 ya walio na virusi hivyo hupata nafuu bila kuhitaji msaada wa matibabu.

 

Makundi yaliyo kwenye hatari zaidi ni yapi?

 

WHO inasema wazee na watu wenye magonjwa ya kudumu kama Shinikizo la Damu, Kisukari, Matatizo ya Figo ndiyo walio kwenye hatari zaidi ya kuathika pindi wanapopatwa na virusi vya Corona. Watu wa umri wa wastani na wenye afya imara wanaweza kupata virusi vya Corona na kupona bila kuhitaji matibabu.

 

Virusi vya Corona vinasambaa vipi?

 


  

Watu wanaweza kupata Virusi vya Corona kutoka kwa watu walioambukizwa. Virusi vinaweza kusambaa kupitia maji maji kutoka kwenye pua au mdomo wa aliyeathirika. Iwapo mtu anagusa maji maji kama mafua, mate na makohozi ya mtu aliye na virusi na kisha kujigusa mdomo, macho na pua anaweza kupata virusi vya Corona.

 

Ninaweza kujikinga vipi na Virusi vya Corona?

 

Nawa vizuri na kila wakati mikono yako kwa maji ya vuguvugu, sabuni au dawa za kuua vijijidudu kwa angalau sekunde 20.

 

Kaa umbali wa angalau hatua mbili (2) kutoka mtu anayepiga chafya au kukohoa.

 

Epuka kushika macho, pua na mdomo kwa mikono isiyo safi kwa sababu mikono hushika sehemu nyingi na ni rahisi kubeba vimelea vya maradhi.

 

Hakikisha wewe, na walio karibu yako wanazingatia ustaarabu wa kuzuia pua na mdomo wakati wa kukohoa au kupiga chafya.

 

Baki nyumbani ikiwa hujisikii vizuri. Iwapo una mafua makali, homa, kikohozi na kushindwa kuhema nenda hospitali kwa sababu huko wataalamu watakupatia msaada muhimu

 

Epuka kuwa sehemu yenye msongamano, kama vyombo vya usafiri, maduka na maeneo yenye yenye mgandamizo wa hewa.

 

Nunua kifunika mdomo na pua na kukikavaa ukiwa kwenye mikusanyiko.

 

Fuatilia taarifa za afya na matangazo yake kuhusu virusi vya Corona.

 

Kwanini watu wanawekwa karantini?

 

Kwa ufupi neno Karantini linamaanisha kuwa chini ya uangalizi. Watu wenye dalili au wanaotokea maeneo yenye maambukizi makubwa ya virusi vya Corona hulazimikwa kuwekwa karantini (kutengwa na watu wengine) ili kufuatilia afya yao kwa karibu na kuzuia kueneza virusi. Ukiambiwa unapaswa kuwekwa Karantini, usiogope. Ni kwa ajili ya afya yako na wengine.

 

Virusi vya Corona vina tiba?

 

Hadi sasa hakuna tiba au chanjo dhidi ya virusi vya Corona lakini kwa sababu virusi hivyo vinaleta dalili mfano wa zile za mafua makali, mchanganyiko wa tiba unatumika kupunguza athari za virusi vya Corona.

 

Ninapaswa kuwa na hofu?

 

Hapana. Hupaswi kuogopa wala kuwa na hofu. Bali unapaswa kuchukua tahadhari. Kila mtu duniani yuko kwenye uwezekano wa kupata virusi vya Corona lakini kama tulivyokufahamisha, athari zake bado hazitishi.

 

Ni kweli watu weusi hawawezi kupata Corona?

 

Hapana, kama ilivyo kwa watu wa rangi na jamii zote sisi watu weusi pia tunaweza kuambukizwa virusi vya Corona. Mfano ni mgonjwa aliyegundulika Arusha.

 


 


read more